IQNA

Hija 1444 H

Saudia yatangaza miongozo jumla kwa Mahujaji ili kurahisisha Hija

20:58 - May 27, 2023
Habari ID: 3477054
TEHRAN (IQNA)- Wizara ya Hija na Umra ya Saudi Arabia imetoa taarifa ya miongozo jumla kwa Mahujaji wa mwaka huu wa Nyumba Tukufu ya Mwenyezi Mungu kwa lengo la kurahisisha ibada hiyo.
Ibada ya Hija ndio mkusanyiko mkubwa zaidi wa Waislamu, ambao hufanyika kila mwaka katika mwezi wa Dhul-Hijjah katika mji mtakatifu wa Makka na kandokando yake nchini Saudi Arabia.
Kwa mujibu wa tovuti ya habari ya Al-Wat'an, katika taarifa yake hiyo, Wizara ya Hija na Umra ya Saudia imesema, ili kurahisisha masuala ya kiidara yanayohusiana na safari, mahujaji wa Nyumba Tukufu ya Mwenyezi Mungu wabebe hati zao rasmi hasa zinazohusiana na amali za Hija na kuchukua mizigo mepesi wakati wa utekelezaji wa amali za Hija.
Wizara ya Hija na Umra ya Saudi Arabia imetangaza kuwa mahujaji wa Nyumba ya Mwenyezi Mungu hawaruhusiwi kuchapisha au kusambaza tarifa za habari bila idhini ya Wizara ya Habari. Aidha wajiepushe kufanya mikusanyiko yenye malengo ya kisiasa.
Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Hija na Umra ya Saudi Arabia, ni marufuku kuweka mikusanyiko kwa ajili ya usomaji dua kwa pamoja.
Kwa mujibu wa miongozo hiyo, Mahujaji wa Nyumba Tukufu ya Mwenyezi Mungu wametakiwa wazingatie pia kwamba ni marufuku kuchukua filamu na kupiga picha ndani ya maeneo matakatifu.

Mahujaji wanatakiwa kubeba nyaraka zote muhimu za kiofisi wanapofika uwanja wa ndege ili kukamilisha taratibu za usafiri. Zaidi ya hayo, wizara imeagiza kuwa kifaa chochote cha kielektroniki kiwekwe ndani ya mizigo iliyokaguliwa.

Mahujaji lazima wahakikishe kwamba kila kipande cha mizigo kitakachosafirishwa kinafuata vipimo vilivyoidhinishwa ili kuhakikisha kuwa kimekubalika. Zaidi ya hayo, alama za utambulisho tofauti zinapaswa kuwekwa kwenye kila kipande cha mizigo kabla ya kusafirishwa.

Wizara ya Hija na Umra ya Saudi Arabia pia imeorodhesha vitu ambavyo ni marufuku, ikiwa ni pamoja na mifuko ya plastiki, chupa za maji, vifaa vya kioevu, na mizigo isiyofunguliwa au kufunguliwa. Sanduku ambazo zimefungwa na kufunikwa kwa kitambaa pia ni marufuku.

Baada ya kuwasili Saudi Arabia, Mahujaji wanatakiwa kutangaza pesa taslimu au vitu vyovyote vya thamani wanavyomiliki vinavyozidi thamani ya SR60,000. Hii ni pamoja na fedha za kigeni, zawadi, vifaa vya kielektroniki, vito na madini ya thamani.

Wizara hiyo imesisitiza zaidi umuhimu wa kujaza tamko la forodha wakati wa kuingia au kutoka Saudi Arabia. Hii ni muhimu hasa ikiwa Mahujaji wanabeba sarafu za ndani au za kigeni, au vitu vyovyote vya thamani ya zaidi ya SR60,000.

Tamko kama hilo la forodha pia linahitajika kwa abiria wanaobeba bidhaa kwa viwango vya kibiashara vya thamani ya zaidi ya SR3,000.

Wizara hiyo imetoa onyo kali kwa mahujaji watakaoshindwa kukamilisha na kusaini tamko la forodha na kubainisha kuwa watawajibishwa.

Inakadiriwa kuwa mwaka huu, Saudi Arabia itapokea Mahujaji zaidi ya milioni mbili, kiasi kwamba mashirika ya ndege ya nchi hiyo yameshatenga tiketi zaidi ya 1,200,000 kwa ajili ya wageni wa Nyumba Tukufu ya Mwenyezi Mungu. Viwanja sita vya ndege vya ndani ikiwa ni pamoja na Jeddah, Riyadh, Al-Dammam, Madinatul-Munawwara, Al-Taif na Yan'ba vitapokea ndege zitakazobeba mahujaji wa mwaka huu.

3483706

Kishikizo: hija saudi arabia
captcha