IQNA

Umuhimu wa Siku ya Quds Duniani katika Mapambano ya Palestina

9:06 - June 30, 2016
Habari ID: 3470425
Ijumaa ya mwisho ya kila mwezi mtukufu wa Ramadhani katika kalenda ya matukio ya dunia, imepewa jina la Siku ya Kimataifa ya Quds.

Mwasisi wa Jamhuri ya Kiislamu hayati Imam Khomeini (mwenyezi Mungu amrehemu) ndiye aliyeipa siku hiyo ya Ijumaa ya mwisho ya mwezi Ramadhani jina la Siku ya Kimataifa ya Quds kwa shabaha ya kuakisi dhulma ya kihistoria inayofanywa na madola ya Magharibi yanayodai kutetea haki za binadamu, dhidi ya watu wanaoendelewa kudhulumiwa na kukandamizwa wa Palestina na ardhi yao takatifu.
Suala la kukombolewa Palestina kutoka kwenye makucha ya Wazayuni maghasibu lilikuwa miongoni mwa malengo na kaulimbiu kuu za Imam Ruhullah Khomeini tangu alipoanza harakati zake hapo mwaka 1960. Wakati huo Imam alikutaja kuasisiwa dola haramu la Israel katika ardhi ya Palestina kuwa ni kitendo cha kishetani na kuutaja utawala huo kuwa ni tezi ya saratani ambalo inapaswa kuondolewa na kukatwa kwa njia yoyote ile inayowezekana.
Baada ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu, wakati ulimwengu wa Kiislamu ulipokuwa bado katika mshtuko wa kutiwa saini makubaliano ya fedheha ya Camp David kati ya aliyekuwa rais wa Misri, Anwar Sadat na waziri mkuu wa wakati huo wa utawala haramu wa Israel Menachem Begin chini ya usimamizi wa rais Jimmy Carter wa Marekani, hatua ya Imam Khomeini ya kuitangaza Ijumaa ya mwisho ya mwezi mtukufu wa Ramadhani kuwa ni siku ya maandamano ya kuhamasisha ukombozi wa Quds tukufu, kwa mara nyingine tena ilihuisha matumaini katika nyoyo za Waislamu. Miezi sita tu baada ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran, yaani tarehe sita Agosti mwaka 1979 sawa na tarehe 13 Ramadhani mwaka 1399 Hijria sambamba na kuanza duru mpya ya jinai na ukatili wa Israel huko Lebanon, Imam Khomeini alitoa taarifa akiitangaza Ijumaa ya mwisho ya kila mwezi wa Ramadhani kuwa ni Siku ya Kimataifa ya Quds na akawata Waislamu kote duniani kuonesha mshikamano wao katika siku hiyo. Katika sehemu moja ya ujumbe wake siku hiyo Imam Khomeini alisema: "Kwa miaka mingi sasa nimekuwa nikiwatahadharisha Waislamu kuhusu hatari ya utawala ghasibu wa Israel ambao sasa na katika siku hizi umezidisha mashambulizi yake ya kikatili dhidi ya ndugu zetu wa Palestina hususa huko kusini mwa Lebanon kwa shabaha ya kuangamiza kabisa wanamapambano wa Kipalestina... Nawataka Waislamu kote duniani na serikali za nchi za Waislamu kushikamana kwa ajili ya kukata mkono wa ghasibu huyo na wasaidizi wake. Vilevile nawaomba Waislamu wote duniani kuichagua Ijumaa ya mwisho ya mwezi mtukufu wa Ramadhani kuwa Siku ya Quds ambayo inaweza kuainisha hatima ya Wapalestina na watangaze mshikamano wa kimataifa wa Kiislamu katika kutetea haki za kisheria za Waislamu wenzao wa Palestina…" mwisho wa kunukuu.
Hatua hiyo ya busara ya Imam Khomeini katika kipindi hicho ilivunja njama za Wazayuni wakiungwa mkono na madola ya Magharibi na viongozi wa nchi kadhaa za Kiarabu kama Anwar Sadat na Mfalme Hussein wa Jordan za kutaka kuutambua rasmi utawala haramu wa Israel.
Kwa upande mwingine mataifa mbalimbali ya Waislamu yalikaribisha hatua hiyo ya Imam Khomeini ya kutangaza Ijumaa ya mwisho ya mwezi wa Ramadhani kuwa Siku ya Kimataifa ya Quds. Waislamu katika mabara yote ya dunia katika kipindi chote cha miaka 37 iliyopita tangu kutangazwa siku hii, wamekuwa wakishiriki kwa wingi katika maandamano ya siku hiyo na kuhuisha pamoja na kuunga mkono malengo ya Wapalestina ya kukomboa Quds tukufu kutoka kwenye makucha ya Wazayuni.
Kwa sasa huko katika Palestina inayokaliwa kwa mabavu utawala wa Kizayuni wa Israel umechukua hatua kali za kiusalama dhidi ya Wapalestina wanaojitayarisha kuadhimisha siku hiyo Ijumaa hii kwa kuwazuia hata kuingia katika Msikiti wa al Aqsa. Katika miaka iliyopita maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Quds huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu yamekuwa yakiandamana na umwagaji damu na makumi ya Wapalestina huuawa kila mwaka katika siku hiyo kwa kupigwa risasi na askari wa Israel na wengine kujeruhiwa. Hata hivyo na licha ya ukatili huo, maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Quds yamekuwa yakifanyika kwa adhama na kwa idadi kubwa zaidi kuliko mwaka wa kabla yake. <<<< >>>>
Moja kati ya maadhimisho makubwa zaidi dunia ya Siku ya Kimataifa ya Quds hufanyika nchini Iran. Wananchi katika miji na vijiji vyote vya Iran huadhimisha siku hiyo kwa maandamano na mikusanyiko wakionesha mshikamano wao na wenzao wa Palestina wanaoendelea kukandamizwa na kusisitiza umuhimu wa kukombolewa Quds tukufu. Wairan hawakuacha kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Quds hata katika kipindi cha mashambulizi ya kinyama ya makombora na ndege za kivita za utawala wa Saddam Hussein. Kushiriki kwa wingi mamilioni ya Wairani katika maandamano ya Siku ya Kimataifa ya Quds ni ishara ya kuendelea kuhuishwa malengo na thamani za Wapalestina za kutaka kukombolewa Quds na nchi yao. Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imekuwa mstari wa mbele daima kuwatetea na kuwasaidia kisiasa, kifedha, kijeshi na kiroho Wapalestina hata katika siku na kipindi kigumu cha mashambulizi ya Wazayuni wa Israel, wakati nchi za Kiarabu zilipowaacha na kuwapuuza Waislamu wenzao wa Palestina hususan wakazi wa Ukanda wa Gaza. Inatupasa pia kuelewa kwamba, kambi ya muqawama na mapambano dhidi ya maghasibu Wazayuni huko Lebanon na Palestina ilianzishwa kwa msaada wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Vilevile ushindi wa mara kwa mara wa wanamapambano wa Lebanon na Palestina mkabala wa Wazayuni huko Lebanon na Gaza ni matunda ya misaada hiyo ya Iran.
Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kamwe haijawahi kuwa na mtazamo wa kimadhehebu au kimakundi katika kuyaunga mkono makundi na harakati za mapambao ya Kiislamu. Kwa mfano tu Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina Hamas inapewa umuhimu na kusaidiwa ipasavyo na Jamhuri ya Kiislamu sawa kabisa na ilivyo kwa harakati ya Hizbullah ya Lebanon. Iran haikubadili kamwe mtazamo na mwenendo wake huo wa kuzisaidia harakati za ukombozi wa Palestina licha ya baadhi ya maafisa wa harakati Hamas kubadili mwelekeo wao na kujitenga kiasi na Jamhuri ya Kiislamu.
Utawala bandia wa Israel na waungaji mkono wake wa Kimagharibi hususan Marekani wanaelewa kwamba, nukta ya udhaifu wa utawala huo ni kambi ya muqawama na harakati za mapambano ya ukombozi wa Kiislamu katika nchi za Syria na Lebanon. Kwa msingi huo walifikia uamuzi kwamba, wanaweza kutimiza malengo yao ya muda mrefu ya kuhalalisha uwepo wa dola bandia la Israel kwa kuanzisha migawanyiko na mpasuko katika kambi hiyo. Wazayuni na washirika wao wamefanya jitihada kubwa katika uwanja huo na kwanza walitumia uwezo wao wote wa kijeshi kuvamia eneo la kusini mwa Lebanon hapo mwaka 2006 kwa shabaha ya kuisambaratisha harakati ya Hizbullah. Hata hivyo mapambano ya kishujaa ya Hizbullah katika vita vya siku 33 na ushindi mkubwa wa wapiganaji wa harakati hiyo viliambatana na kushindwa kihistoria kwa utawala bandia wa Israel. Wakati huo huo ushindi wa wapiganaji wa Hamas mbele ya uvamizi wa Israel katika eneo la Gaza hususan uwezo wa makombora ya harakati hiyo wa kupiga maeneo ya Tel Aviv, vimeonesha tena ni kwa kiwango gani Israel inakabiliwa na changamoto kubwa. Ni kutokana na kushindwa na changamoto hizo ndipo kukaanzishwa mradi wa kuzusha ghasia na vita vya ndani nchini Syria kwa kutumia kisingizio cha kuimarisha demokrasia na kuiondoa madarakani serikali halali ya nchi hiyo. Watekelezaji wakuu wa mradi huo ni Saudi Arabia, Uturuki na Qatar wakisaidiwa na Israel na nchi kadhaa za Magharibi hususasn Marekani. Mradi huo ulianzishwa kwa shabaha ya kusambaratisha kambi ya muqawama na mapambano ya ukombozi dhidi ya Israel na kuliondoa kabisa suala la kukaliwa kwa mabavu Palestina katika ajenda kuu ya ulimwengu wa Kiislamu. Katika fremu hiyo yalianzishwa na kuimarishwa makundi ya kigaidi na kitakfiri kama Daesh na Jabhatu Nusra katika nchi za Syria na Iraq ambayo sasa yamekuwa tishio kubwa kwa ulimwengu wa Kiislamu. Mgogoro huo umesababisha vifo vya maelfu ya watu na kuwalazimisha mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi.
Sera na siasa hizo za utawala bandia wa Israel na washirika wake za kuzishughulisha nchi za Kiislamu na kuzusha migogoro ya ndani zimewafanya walimwengu wasahau au kuyapa umuhimu ndogo maudhui ya Palestina na masaibu wanayoendelea kukutana nayo watu wa Palestina. Siku ya Kimataifa ya Quds ni cheche na chachu inayowaamsha Waislamu na wapenda haki kote ulimwenguni na kuwataka waelewe kwamba, chanzo cha migogoro na matatizo mengi ya ulimwengu wa Kiislamu na Mashariki ya Kati ni utawala bandia na haramu wa Israel. Kwa msingi huo nchi za Waislamu hazitapata ustawi, amani na maendeleo maadamu utawala bandia wa Israel ungalipo na unaendelea kuungwa mkono kwa hali na mali na washirika wake wa Magharibi na vibaraka wao kama Saudi Arabia, Uturuki n.k.

captcha