Sheikh Ali al-Qaradaghi amesema katika taarifa yake kwamba vitendo hivyo ni jinai na dhambi na kusisitiza kuwa, kulenga maeneo ya kidini na kuua watu wasio na hatia ni kinyume na mafundisho ya Uislamu na dini nyingine zote.
Alisema msimamo usiobadilika wa IUMS ni kukataa unyanyasaji na ugaidi na kuzingatia vitendo hivyo kuwa ni uhalifu bila kujali ni nani anayevifanya na sababu gani zinaweza kuwa.
Ameendelea kwa kushiria sehemu aya ya 32 ya Surah Al-Ma'idah katika Qur'ani Tukufu isemayo “…aliye muuwa mtu bila ya yeye kuuwa, au kufanya uchafuzi katika nchi, basi ni kama amewauwa watu wote. Na mwenye kumuokoa mtu na mauti ni kama amewaokoa watu wote…"
Sheikh Qaradaghi aidha amezitaka nchi zote za dunia kushirikiana katika kuhakikisha usalama na amani na kupambana na ugaidi wa aina zote hususan ugaidi wa serikali wa utawala wa Kizayuni wa Palestina.
Maulamaa watatu walishambuliwa na mshambulizi mwenye umri wa miaka 21 kwenye Haram Takatifu ya Imam Ridha AS, wiki iliyopita. Wasomi hao wa Kiislamu walikuwa wamejitolea kutoa huduma katika haram hiyo takatifu wakati wa mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Wawili kati ya maulamaa hao waliuawa shahidi na mmoja kujeruhiwa kutokana na shambulio hilo.
Mshambulizi huyo, aliyetambuliwa katika vyombo vya habari vya ndani kama Abdol Latif Moradi, raia wa Afghanistan mwenye umri wa miaka 21 ambaye aliingia Iran kinyume cha sheria kutoka Pakistan mwaka jana, aliwekwa chini ya ulinzi wa polisi mara moja.
Video zilizosambaa kwenye mitandao ya kijamii zilionyesha kuwa alikuwa chini ya ushawishi wa itikadi za kitakfiri na kundi la kigaidi la Daesh au ISIS.
Hujuma hiyo ya kigaidi inaendelea kulaaniwa kote duniani.