Balozi al Zawawi alikuwa miongoni mwa waanzilishi wa harakati ya Fat'h na alikuwa Balozi wa Palestina hapa mjini Tehran kwa muda wa miaka 39.
Aliacha kazi hiyo ya ubalozi mwaka jana 2022 na kumpisha binti yake Salam al Zawawi kushika nafasi ya balozi wa Palestina hapa nchini Iran.
Hossein Amir-Abdollahian, Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema katika ujumbe wake wa maandishi wa jana Jumatatu kwamba, marhum, Salah al Zawawi alikuwa mpambanaji shupavu kwa miaka mingi na muda wote walikuwa mstari wa mbele katika mapambano ya ukombozi wa ardhi za Palestina. Alibeba jukumu la kidiplomasia la Palesina kwa ajili ya kupigania haki za taifa hilo madhlumu na kubakisha hai malengo matukufu ya Palestina.
Vile vile ameandika kwenye ujumbe huo wa tanzia kwamba: Ni matumaini yangu, karibuni hivi tutashuhudia matunda ya jitihada na mapambano ya miongo kadhaa ya wananchi wa Palestina yakiwemo ya marhum Salah al Zawawi na tutashuhudia ardhi zote za Palestina zikikombolewa kutoka kwenye makucha katili ya Wazayuni, na kutoa fursa ya kuundwa serikali yenye nguvu ya Palesitna ambayo mji mkuu wake ni Quds Tukufu (Jerusalem).
Salah al Zawawi, alikuwa balozi wa pili wa Palestina nchini Iran baada ya Hani al-Hassan. Mwanadiplomasia huyo pia aliwahi kuwa balozi wa Palestina huko Algiers, Brazil na Kenya.
Aliitwa Sheikh al-Sufara (kiongozi wa mabalozi) kutokana na kuwepo kwake kwa muda mrefu kama balozi wa Palestina nchini Iran.
4123420