Tokea mwaka 2011, Waislamu mjini Memphis wamekuawa wakiandaa hafla kadhaa kwa lengo la kustawisha uelewa wa Uislamu na pia kuwawezesha wasiokuwa Waislamu kuwa na maingiliano mema na Waislamu.
Kaulimbiu ya sherehe za mwaka huu ni "Kudumisha Uanadamu Wetu Katika Zama za Kisasa".
Sherehe hizo ambazo zilianza Jumamosi Pili Machi zinafanyika katika misikiti kadhaa ambayo milango yake iko wazi kwa wageni ambao wanaelekezwa na kupewa mafunzo kuhusu historia ya Uislamu.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Waislamu wa Mji wa Memphis Isam Abu-Khraybeh anasema, "Iwapo unataka kuujua Uislamu halisi, unapaswa kuwasikiliza Waislamu badala ya kutegemea vyombo vya habari ambavyo wakati mwingi hueneza propaganda na hadaa tupu. Aidha kuna watu ambao wanatafsiri binafsi za Uislamu na zinaweza kuwa si sahihi."
Kampeni hiyo inakuja huku kote Marekani kulishuhudiwa ongezeko la chuki dhidi ya Waislamu kutokana na sera za kibaguzi za mtawala wa nchi hiyo, Donald Trump.
Wakati wa kampeni zake, Trump alikuwa ametaka Waislamu wazuiwe kikamilifu kuingia Marekani na punde baada ya kuingia madarakani alipitisha amri ya kuwapiga marufuku Waislamu kutoka nchi kadhaa kuingia nchini humo.
Baraza La Mahusiano ya Kiislamu Marekani (CAIR) linasema tokea Trump achaguliwe kuwa rais wa Marekani, Waislamu nchini humo wameshuhudia ongezeko kubwa la ubaguzi dhidi yao huku wakishambuliwa na kubugudhiwa na watu wenye chuki dhidi ya Uislamu.