Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, Bi.Ginella Massa alitakiwa kusoma taarifa ya habari ya saa tano usiku Ijumaa katika Televisheni ya City News na punde baada ya habari kulizika wimbi la maoni katika mitandao ya kijami huku yeye binafsi akiandika katika akaunti yake ya Twitter kuwa: "Usiku huu si tu kuwa ni muhimu kwangu binafsi. Sidhani kuna mwanamke ambaye ameshawahi kusoma taarifa ya habari katika televisheni Canada akiwa amevaa Hijabu."
Massa mwenye umri wa miaka 29 aliweka historia mwaka 2015 kama mwandishi habari wa kwanza kuvaa Hijabu Canada wakati akiwa ripota wa televisheni ya CTV News huko Kitchene, Ontario. Alirejea Toronto na kupata kazi katika televisheni ya CityNews.
Massa anasema hakutambua umuhimu wa usiku huo hadi pale alipomaliza kusoma habari na mhariri wake alipoashiria kuwa alikuwa ameweka historia.
"Mhariri wangu aliniambia, 'ilikuwa kazi nzuri! Hiyo ilikuwa mara ya kwanza Canada? Mwanamke akiwa amevaa Hijabu?' Nami nikasema naam. Kisha nikaandika kuhusu tukio hilo katika twitter. Pamoja na kuwa nilifahamu umuhimu wa tukio hilo, sikutaraji kupokea maoni mengi kiasi hicho. Simu yangu haijaacha kuita tokea wakati huo."
Mafanikio hayo yanakuja huku kukiwa na ongezeko la vitendo vya chuki dhidi ya Waislamu katika nchi jirani ya Marekani na Ulaya. Katika kampeni zake, mshindi wa kiti cha urais Marekani Donald Trump alitishia kuwazuia Waislamu kuingia Marekani.
"Nimezungumza na wanawake Waislamu waandishi habari nchini Marekani na wamenifahamisha kuwa wanakabiliwa na changamoto chungu nzima wakijaribu kuchukua kazi za kutangaza habari katika televisheni."
Anasema anasikitika kwani wengi wamefahamishwa wazi wazi kuwa hawawezi kutangaza habari kwa sababu tu wanavaa Hijabu.
Ingawa Massa amesifiwa na wengi na kupokea maoni
mazuri nchini Canada anasema pia kuna watu wachache waliotoa maoni yasiyo
mazuri lakini anasema hilo halimvunji moyo kwani umma unapaswa kuonyeshwa
taswira chanya za mwanamke Mwislamu.