IQNA

Maandamano ya kumuunga mkono Sheikh Zakzaky Yafanyika nchi mbali mbali

14:24 - April 16, 2018
Habari ID: 3471467
TEHRAN (IQNA)-Wanaharakati katika maeneo mbali mbali duniani Jumapili wameshiriki katika maandamano ya kutangaza kufungamana kwao na Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria Sheikh Ibrahim Zakzaky ambaye anashikiliwa kinyume cha sheria nchini humo.

Kwa mujibu wa taarifa, maandamano hayo yalifanyika Uingereza, Pakistan, Uturuki, Uswisi na Indonesoa ambapo washiriki wamelaani vikali hatua ya serikali ya Nigeria kuendelea kumshikilia Sheikh Zakzaky huku wakitaka aachiliwe huru mara moja.

Mjini London, maandamano yamefanyika mbele ya Ubalozi wa Nigeria huku mjini Geneva, Uswisi waandamanaji wakikisanyika mbele ya Ofisi ya Umoja wa Mataifa.

Itakumbukwa kuwa Sheikh Ibrahim Zakzaky akiwa na mke wake walitekwa nyara na Jeshi la Nigeria mwezi Disemba mwaka 2015 wakati askari walipovamia kituo chake cha kidini huko katika mji wa Zaria jimboni Kaduna. Tokea wakati huo Sheikh Zakzaky na mkewe wamekuwa wakizuiliwa katika mojawapo ya vituo vya kijeshi vya nchi hiyo bila kufunguliwa mashtaka.

Uvamizi huo ulijiri baada ya Jeshi la Nigeria kudai kuwa wafuasi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria walikuwa na njama ya kutaka kumuua mkuu wa jeshi hilo, madai ambayo yalikanushwa vikali na wafuasi wa harakati hiyo.Inakadiriwa kuwa Waislamu 1000 wasio na hatia waliuawa katika tukio hilo .

3465529

captcha